Friday, February 14, 2020

VITU KUMI HATARI KWA AJILI YA SAUTI YAKO.


An ink wood engraving from 1875 - showing the anatomy of a human larynx


Nakushukuru ndugu msomaji wangu kwa kuendelea kufuatilia makala hizi. 

Nilikuwa naongea na Tabibu kutoka Hospitali ya wilaya ya Chato, Paul. M.Kahindi kuhusu jinsi ya kutunza sauti zetu na madhara yanayoweza kutokea na kuharibu sauti zetu baada ya kutumia baadhi ya vitu, tabia ama matibabu. Namshukuru sana huyu tabibu na Mungu ambariki sana na aendelee kummiminia neema na baraka zake katika kazi zake.

Kuimba, kuongea nakutumia sauti kwa mambo mbalimbali ni kipaji na ni wito. Mungu ndiye anayegawa kipaji hiki lakini kila mmoja anaweza kuimba ilimradi tu anajua kuongea, ukijifunza au kufundishwa vizuri jinsi ya kuimba. 

Swali ni kwamba; Unaweza kuwa mtu ambaye unaongea sana, muimbaji au mcheshi lakini ni kwa kiasi gani unaifahamu sauti yako hiyo ambayo ni nzuri na inayofurahisha na kustastaajabisha, ukilipata jibu hapa basi unaweza kuungana na mimi katika harakati za kuitengeneza sauti yako iweze kudumu katika ubora wake.

Watoto huwa wanaakisi lafudhi za wazazi wao wakati wakiwa bado tumboni
Watafiti waliwachunguza watoto waliozaliwa Ufaransa na Ujerumani na kubaini kuwa kile kilio ambacho huwa wanakitoa wakati wanazaliwa huwa ndio lugha ya mama zao na wameonyesha pia namna ambavyo inawezekana kujua watoto hawa wametoka mataifa tofauti kwa namna ambavyo wanalia

Sauti huwa inajihifadhi katika sehemu maalum ndani ya mwili wako. Sauti yako inaanzia kutoka ndani, ukiwa unahema taratibu huwa inaendeshwa na sanduku linalohifadhi sauti (voice box), Vipande viwili vya tishu hutikisika kwa kwenda mbele na kurudi nyuma wakati ambapo hewa inapita mdundo wa sauti unatengenezwa.

Kama wewe ni Mwanakwaya, mwimbaji, msanii au mshereheshaji  au ni mtu unayehitaji kutumia sauti yako kuongea na kundi fulani la watu, kuimba au kwa chochote, nakushauri utunze sana sauti yako kwa kuzingatia mambo muhimu kwa ajili ya kutunza sauti na kuifanya idumu kwa ubora mpaka Mungu atakapokuita kutoka hapa duniani. Kwa maana hiyo, ni lazima kwa makundi ya watu niliyoyasema hapo juu kuwa makini na vyakula, vinywaji na mfumo wa maisha tunayoishi ili kuepuka tatizo la kuharibu sauti yakomaana sauti hii tunayoiongelea leo inaweza kukupatia pesa na faida zingine kwako binafsi,  kwa Mungu, kwa jamii na kwa serikali pia. (Tumia sauti yako kama mtaji wako!)


 VITU KUMI HATARI KWA SAUTI YAKO


Kuna vitu vingi sana vinavyoweza kuharibu sauti yako ewe msanii wa sauti (mwanakwaya, mwimbaji, msanii na mtoa hotuba) lakini kwa leo nitakuelezea vitu kumi. 

Kama nilivyokueleza hapo juu kuhusu jinsi inavyotengenezwa sauti na umuhimu wa kuitunza sauti yako, unatakiwa kuzingatia mambo yafuatayo ili sauti yako iwe vizuri na kwenye ubora usioharibika;

  1. POMBE.  Pombe ni kinyaji kizuri sana kwa ajiri ya kuburudisha akili na ubongo wa mwanadamu kwa ujumla, lakini ina madhara makubwa sana kwa afya ya msanii, mwanakwaya, mshereheshaji na watu wengine wanaotumia sauti zao kuongea na jamii kwa njia yoyote ile.Pombe huongeza saizi na kubadilisha muonekano wa mapafu na mfumo wa sauti kwa ujumla. kwa maana hiyo, pombe huharibu sauti ya mwimbaji au mfikisha taarifa/ujumbe kwa njia ya sauti kwa kuharibu mfumo wa utendaji kazi wa mapafu. lakini pia pombe huchoma koo kwa kilevi kilichomo na baadae husababisha kansa ya koo. (Hii ni hatari sana kwa mwimbaji na kwa jamii pia)  (ILI KUTUNZA SAUTI YAKO, ACHA KABISA KUNYWA POMBE.)

  1. Matumizi ya dawa kwa muda mrefu. Sote tunajua kuwa, ili sauti iwe vizuri, unatakiwa kuwa na afya njema sana kila wakati. Dawa ni sumu na ina tindikali pia (kwa baadhi ya dawa) na   inaweza kuharibu chochote katika mfumo wa afya ya mwanadamu. Matumizi ya dawa ya muda mrefu husababisha kuuawa kwa kinga mama za mwili (self immunit) Mfano. Matumizi ya Chrolomphenicol kwa muda mrefu husababisha madonda mdomoni na hii inaweza kusababisha upweke na kujitenga kwenye kundi la watu au kushindwa kutimiza jukumu lako kwa wakati muafaka)  


  1. Matumizi ya sigara: Kama nilivyokueleza hapo juu, sigara pia ina tindikali (Nicotin) ambayo huingia katika mfumo wa hewa (trachea, mapafu , Vocal cord) na husababisha ukungu katika mapafu na mfumo wa sauti kwa ujumla. Lakini pia,  ukungu husababisha msukumo wa damu kuwa mkubwa zaidi na kusababisha kupasuka kwa mishipa inayosafirisha damu kutoka kwenye moyo kwenda kwenye mapafu, hii hali ikitokea husababisha hata mtu kutapika damu kwa kuwa mshipa huo umeshapasuka. Hii hutokea pia hata kwa wananokunywa pombe sana na wanaotumia madawa mbalimbali ya kulevya.

  1. Matibabu ya upasuaji wa koo. Hii pia ni tatizo kwa waimbaji japo siombei mtu kufanyiwa upasuaji. Mtu aliyefanyiwa upasuaji wa koo ana shida katika utoaji wa sauti. Mtu huyu kama yupo kwenye kikundi fulani, anatakiwa kupewa ruhusa kwenye baadhi ya mazoezi katika uimbaji.


  1. Ulaji wa vyakula vya baridi sana, vya moto sana au vyenye tindikali kama limao n.k., Ulaji wa vyakula hivi husababisha madhara kwa msanii, mwimbaji, msemaji  kwa sababu, vyakula vya baridi hubadilisha hata mfumo wa sauti. Vyakula vya moto huchoma  koo na kusababisha kuuawa kwa baadhi ya seli za mwili na hivyo kuharibu mfumo mzima wa sauti.

  1. Maambukizi katika njia ya koo. (KOO NDILO MTAJI KATIKA SAUTI), na kama tunatambua hilo,tumeshajua umuhimu wa koo katika kazi hii ya kuwasiliana na jamii kwa njia mbalimbali kama za nyimbo, kwaya, kuongea n.k


  1. Ugonjwa wa koo; Watu wenye magonjwa ya koo wanapata shida sana katika kuimba au  kuongea na hadhira. sitawaongelea sana hawa watu kwa siku ya leo, lakini pia, ugonjwa huu huathiri sauti kwa kiwango kikubwa.

  1. Matibabu ya mionzi kwenye koo; Nakuomba ndugu yangu ambaye kipaji chako ni kufikisha ujumbe wako kwa hadhira kwa njia ya sauti, usipende sana matibabu haya japo yakihitajika ni lazima ufanyiwe tu. Matibabu haya husababisha sauti kubadilika kutoka kwenye uhalisia.


  1. Kurithi; Kuna matatizo mengine ya kurithi yanayoweza kusababisha sauti yako kuwa mbaya, matatizo haya yanaweza kuwa ya kiakii, kisaikolojia n.k. Mtoto huwa anarithi sauti ya mzazi wake tangu akiwa tumboni na hata akizaliwa, sauti anayoitoa wakati analia ni uhalisia wa sauti ya mama yake. Kwa maana hiyo, mtoto huyu anaweza kurithi sauti kutoka kwa mzazi wake.

  1. Kupiga kelele na kufanya kazi zinazoambatana na kupiga kelele; Kuna baadhi ya sekta za kiserikari na binafsi huwa na utaratibu wa kupiga kelele mara kwa mara kama jeshini, (mf. Mguuuuuuu pandeee!), wapiga debe stendi n.k Watu hawa huishi kwa sauti hizo walizozizoea, kwa hiyo kama atakuwa ni msanii ataitumia sauti yake kwenye kipaji chake na wakati mwingine atatumia hata kwenye maongezi. Hili nadhani kila mtu analijua na tunaliona katika jamii inayotuzunguka.


Hayo ndiyo mambo niliyokuandalia leo lakini tujue kuwa uongeaji wetu, Uimbaji wetu na kipaji chetu kinatakiwa kuakisi yale tunayoyaishi. 




Imeandikwa na; 
Emmanuel W Shimbala
Katibu
SEM BAND TANZANIA
CHATO-GEITA TANZANIA
+255 762 176 662 au +255 756 446 979
E-mail: sembandtanzania@gmail.com


Wednesday, February 12, 2020

FAIDA ZA KUIMBA KWA AFYA YAKO



Habari za leo ndugu msomaji wa SEM-BT?


Leo nitaongelea kuhusu faida za kuimba ambazo zinamsaidia mtu kiafya.

Kwanza kabisa naomba nikueleze maana ya kuimba.

KUIMBA ni kutoa sauti yenye ulinganifu, sauti hiyo inatakiwa kufuata mapigo ya ki muziki na ni zaidi ya kughani. Zamani mababu zetu walikuwa wanaimba kwenye kazi mbalimbali ili kurahisisha kazi yenyewe iliyokuwa ikifanyika, mpaka sasa watu wengi huimba ili kuburudisha, kufundisha, kukosoa au kuelimisha kikundi fulani cha watu.

Kuimba ni faida kwa mwimbaji kwani kuna faida nyingi saana ambazo mwimbaji anazipata kama vile kuburudika, kuburudisha, kuinjilisha, kuhamasisha, kufariji, kufurahisha n.k

Leo nitakueleza faida za kuimba ambazo zinamsaidia mwimbaji kiafya, Faida zenyewe ni:

  1. Kuimba ni mazoezi. Unapoimba unafanya mazoezi ambayo pia ni kinga kwa magonjwa mbalimbali yanayoweza kumuathiri mtu ambaye hafanyi mazoezi. Mazoezi ambayo nayasemea hapa ni Kupanua kiwambo (diaphragm), mwanakwaya anatumia nguvu nyingi sana wakati anaimba ili kupanua mapafu na kiwambo. Hii itamsaidia mwimbaji ku zuia magonjwa yanayoweza kuathiri mapafu kama vile kikohozi, mafua.
  2. Inasaidia kuboresha mfumo wa upumuaji mwilini kwani msukumo wa damu utakuwa mkubwa ambapo ndani ya chembe za damu huwa kuna hewa safi ya Oxygen ambayo husambazwa mwilini pote na chembe za damu katika mzunguko. 
  3. Inasaidia kupunguza mawazo. Hili liko wazi kabisa  kwa mwanakwaya au mwimbaji yeyote yule, ukiimba unapunguza mawazo. Mtu mwenye mawazo anaweza kuugua hata magonjwa ya akili na kisaikolojia.
  4. Husaidia kusimama vizuri. Mwimbaji huwa ana staili yake ya kusimama ambapo kifua chake anakiweka mbele, mabega yanakuwa yameinuka kidogo ili kumsaidia kutoa sauti, mgongo pia unakuwa umenyooka vizuri. Hii inamsaidia kuufanya uti wa mgongo usijikunje. Kwa hiyo mwanakwaya anapoimba kwa muda mrefu huwa na tabia ya kusimama kama anataka kuimba na hivyo kumsaidia yeye kutunza na kukinga uti wa mgongo.
  5. Huimarisha mfumo wa kinga mwilini. (strengthen the immunity system) Kwenye      mwili wa binadamu kuna kinga (protini) ambayo ina jina la kitaalamu ambalo ni Immunoglobulins, kwa hiyo mtu anapoimba anafanya mazoezi (kama nilivyosema hapo juu) na unapofanya mazoezi ina maana kwamba unaongeza kinga mwilini tofauti na mtu ambaye amekaa tu bila kufanya mazoezi



Kwa ufupi sasa kuimba kuna faida kiafya, faida zingine nimezitaja hapa chini ambazo ni:

  • Kuimba nidawa ya asili ya mawazo (natural annti-depresant)
  • Kuimba kunapunguza mawazo kwa kiasi kikubwa sana (ni dawa kwa mtu mwenye mawazo)
  • Kuimba kunaongeza uwezo wa kufikiri na kuchukua maamuzi.

Faida za kuimba kwenye jamii.


  1. Kuimba humsaidia mtu kuongeza idadi ya marafiki.
  2. Kuimba kunamwongezea mtu kujiamini katika kila kitu anachokifanya kwa faida yake na jamii kwa ujumla.
  3. Kuimba kunapanua wigo wa mawasiliano.
  4. Kuimba humsaidia mtu kuwa na hisia juu ya kile anachokiimba.
  5. Kwa wanakwaya wa nyimbo za dini, kuimba kunamweka karibu na Muumba wake.
Kwa leo naomba niishie hapo, nakutakia kila la heri katika majukumu mbalimbali ya kujenga taifa na jamii yetu kwa ujumla. Nakuomba pia uendelee kuka mkao wa kusubiria kazi ambayo tutaitoa hewani muda si mrefu, ni nyimbo mbili ambazo tulizirecord kwa mfumo wa sauti na video.


Imeandikwa na;
SEM BAND TANZANIA
CHATO-GEITA TANZANIA
+255 762 176 662 au +255 756 446 979
E-mail: sembandtanzania@gmail.com 


Monday, February 10, 2020

KUHUSU SEM-BT



Karibu sana mpenzi msomaji wangu na leo nakuletea utambulisho wa kikundi kidogo cha SEM-BT.

SEM-BT ni kikundi cha watu wachache ambacho kinatoa huduma zake hapa tanzania

Kikundi cha SEM BAND – TANZANIA (SEM-BT) ambacho kimesajiliwa kisheria kwa namba za usajili CDC/CSO/114/2019, ambacho makao makuu yake ni Chato kati karibu na ilipokuwa ofisi ya TANESCO, kinajishughulisha na shughuli  za kuandaa matamasha mbalimbali ya  uimbaji wa nyimbo ikiwa ni pamoja na kuziweka katika mfumo wa sauti na Video na kuuza DVD ili kujipatia kipato. Pamoja na kuwaunganisha vijana kuwa pamoja katika shughuli mbalimbali za kiuchumi, kidini na kijamii.

Kikundi hiki kilianzishwa tangu mwaka 2016 ambapo kilikuwa na watu wawili tu na kazi zake ilikuwa ni kuwaunganisha watu mbalimbali katika matamasha mbalimbali ya kidini na kijamii. kikundi hki hakikuweza kuendelea zaidi kutokana na kukosa pesa za kuendeshea kikundi. Mwaka 2019 waasisi wa kikundi hiki waliamua kushirikisha wadau wengine ili kuweza kurekodi na tulifanikiwa kurekodi nyimbo mbili kwa mfumo wa sauti na video pia (Nyimbo hizo ni ("Basi iweni na huruma" uliotungwa na E.Ogeda pamoja na "Tuwe na moyo wa majitoleo" uliotungwa na E.Nyanza). Mpaka sasa hivi tunajiandaa kuzisambaza hizo nyimbo zetu kwa njia ya you tube na mitandao mingine ya kijamii muda si mrefu. kaa tayari kuzipokea.

Endelea kutufuatilia kwani tutakuletea mambo mengi mazuri kwa siku zinazokuja.

Emmanuel. Shimbala
Katibu SEM-BT

VITU KUMI HATARI KWA AJILI YA SAUTI YAKO.

Nakushukuru ndugu msomaji wangu kwa kuendelea kufuatilia makala hizi.  Nilikuwa naongea na  Tabibu kutoka Hospitali ya wilaya ya C...